BONYAD AKHTAR TABANELIMU YA KIISLAMU

Imamu Sadiq (amani iwe juu yake) ni shujaa wa wito wa Umoja wa Kiislamu

Utaratibu na Mpangilio:  Bonyad Akhtar Taban

Imamu Sadiq (amani iwe juu yake) ni shujaa wa wito wa Umoja wa Kiislamu

Tunapenda kutoa pole kwa Waislamu wote, hususan wafuasi wa Ahlul-Bayt(a.s) katika kumbukumbu hii ya kuuawa kishahidi Imam Ja’far Ibn Muhammad al-Sadiq (as).

Katika mnasabat huu, tungependa kuangazia umuhimu wa Umoja wa Kiislamu kama ulivyoamrishwa na kutekelezwa na Imam Sadiq (a.s), Mjukuu wa Mtume Muhammad (s.a.w.w):

Imam huyu Mtukufu, Imam Ja’far Ibn Muhammad al-Sadiq (a.s) – alikuwa na fursa pana zaidi kuliko Maimam wengine katika maisha yake ya kufikisha mafundisho ya Nyumba Tukufu ya Mtume Muhammad(s.a.w.w) – ambayo kwa hakika ni mafundisho safi ya Kiislamu – kuelekea mioyo safi ya wale wenye shauku ya kupokea maarifa safi ya Kiislamu, na waliokuwa na kiu ya mafundisho ya Ahlul-Bayt(a.s).

Ni makosa makubwa kudhani kwamba maelfu ya wanafunzi wa Imam Sadiq(a.s) na watu wote waliofundishwa na Imam huyu mwema, walikuwa Waislamu wa Madhehebu ya Shia na ambao waliamini kuwa yeye ni Imam kwao. La hasha! suala la msingi katika mafundisho yake halikuwa katika mwelekeo huo. Imam (a.s) alikuwa akifunza maarifa ya dini kwa waislamu wote wanaomkubali na kuamini yeye ndiye Imam wao na Kiongozi wao, na hata wale ambao hawakuwa miongoni mwa wafuasi wake.

Kwa maana kwamba: Kulikuwa na watu wengi miongoni mwa wanafunzi wake ambao hawakuamini – jinsi Waislamu wa Madhehebu ya Shia wanavyoamini – kwamba yeye ni Imam katika silsila ya Maimam kumi na wawili (a.s), lakini walikuwa wakienda kwake ili kufaidika na elimu yake na yale anayoyajua kuhusu mafundisho matukufu ya Kiislamu.

Katika vitabu mbalimbali vya Shia Ithna Ashari na Ahlu- Sunna, kuna hadithi nyingi kutoka kwa Imam Sadiq (a.s) ambazo zimesimuliwa na Waislamu wa Sunni – kwa maana:  Waislamu wasiokuwa wa Madhehebu ya Shia Ithna Ashari.

Hii inaashiria kwenye ukweli huu usiopingika kwamba Umma wa Kiislamu na ulimwengu wa Kiislamu bado unahitaji mafundisho ya Imam Sadiq (a.s) na Maimamu wengine(a.s). Ni lazima waislamu wote wanufaike na mafundisho haya ya Imam Sadiq(a.s) na Maimam wa Ahlul – Bayt (a.s) kwa ujumla.

Wanachama wa Umma wa Kiislamu kutoka tabaka mbalimbali za kijamii hawana budi kuongezana katika elimu zao na maarifa yao njia hii ili waweze kuinua zaidi na kuboresha kiwango cha mafundisho ya Kiislamu, jambo ambalo litatulazimu tuepuke kujenga ukuta wa uadui na chuki baina ya Waislamu wa madhehebu mbalimbali.

Na tunaposema Umoja wa Kiislamu, basi hivyo ndivyo tunavyomaanisha, kwamba huu ndio Umoja wenyewe wa Kiislamu.

Na hivi ndivyo Imam Sadiq (a.s) alivyoujenga na kuuimarisha Umoja wa Kiislamu kupitia kusambaza Sayansi na Maarifa ya Kiislamu kwa Waislamu wote. Leo hii kuna vinara wakubwa katika ulimwengu wa Ahlu-Sunna wal Jamaa, ambao ukitizama elimu yao wametoa kwa Imam Jaafar Sadiq(a.s), bali ni wanafunzi miongoni mwa wanafunzi wake.

Related Articles

Leave a Reply

Back to top button
×